Vyombo vya habari endeleeni kutoa elimu ya unyonyeshaji maziwa ya mama

News Image

Imewekwa: 4th Aug, 2023

Mkurugenzi Mtendaji Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania, Dkt. Germana Leyna akifungua semina ya waandishi wa habari mkoa wa Dar es salaam kuhusu Maadhimisho ya Wiki ya Unyonyeshaji wa Maziwa ya Mama kwa mwaka 2023 iliyofanyika 03/08/2023 katika ukumbi wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania jijini Dar es Salaam.

Imeelezwa kuwa vyombo vya habari vinamchango mkubwa katika kutoa taarifa sahihi kuhusu unyonyeshaji na ulishaji wa watoto kwa ujumla na kusaidia kupambana na imani potofu kuhusu unyonyeshaji na taarifa zisizo sahihi zinazolenga maslahi ya kibiashara ya maziwa mbadala na vyakula vya watoto wachanga na hivyo kuchangia uboreshaji wa lishe na afya ya mama na @mtoto na kujenga taifa lenye nguvu imara na yenye tija.

Hayo yamebainishwa na Mkurungezi Mtendaji wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania Dkt. Germana Leyna, wakati wa semina elekezi kwa waandishi wa habari mkoa wa Dar es Salaama, kuhusu umuhimu wa kuandika, kuhabarisha na kuelimisha jamii kuhusu masuala mbalimbali yanayohusiana na lishe na afya ikiwa ni mwendelezo wa shughuli mbalimbali zinazofanyika katika kuadhimisha Wiki ya unyonyeshaji wa maziwa ya mama Duniani.
Dkt. Germana amesema vyombo vya habari vina wajibu wa kuendelea kutoa taarifa na kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa kufuata taratibu sahihi za unyonyeshaji wa maziwa ya mama, kwani ni miongoni wadau wakuu wa mawasiliano yanayolenga kubadili mitazamo na tabia za jamii kuhusu masuala ya lishe na afya.
“vyombo vya habari vina mchango mkubwa katika kutoa taarifa, kuelimisha na pia kuburudisha na miaka ya hivi karibuni dhima hiyo imepanuka na kujumuisha masuala ya ufuatiliaji, kupaza sauti za watu wasio na sauti katika jamii, kusaidia kulinda maslahi katika jamii na mambo mengine” Alisema Dkt. Germana
Kwa upande mwingine Dkt. Germana amesisitiza juu ya waajiri katika sekta rasmi na zile zisizo rasmi, kuchukua hatua za kuboresha mazingira ya kazi na msaada unaofaa katika kufanikisha unyonyeshaji mahali pa kazi kama nyenzo muhimu ya kuwezesha wanawake waliopo kazini kupata fursa ya kunyonyesha watoto wao na kuendelea na kazi zao.
Nchini Tanzanaia maadhimisho ya Wiki ya unyonyeshaji maziwa ya mama nchini yalianza kuadhimishwa mwaka 1992, ambapo huambatana na shughuli mbalimbali zinazolenga kufikisha taarifa, jumbe na hamasa kwa wananchi kuanzia ngazi ya Mkoa, Halmashauri na kwenye jamii.